IQNA

Khatibu wa Sala ya Ijumaa Tehran

Kisingizio kilichotumiwa na wafanya fujo Iran ni cha ajabu sana

20:39 - September 23, 2022
Habari ID: 3475826
TEHRAN(IQNA)- Khatibu wa Sala ya Ijumaa ya Tehran Hujjatul Islam Sayyid Ahmad Khatami amesema kwenye khutba za Sala ya Ijumaa kwamba, kufariki dunia mwananchi yoyote Iran jambo la kusikitisha na inabidi kuipa mkono wa pole familia ya marehemu.

Khatibu wa Sala ya Ijumaa alikuwa akiashiria kifo cha Mahsa Amini ambaye alifariki hivi karibuni.

Mnamo Alkhamisi iliyopita ya tarehe 15 Septemba, na kufuatia kutangazwa habari ya kubadilika ghafla hali ya kiafya ya kijana mmoja wa kike, Idara ya habari ya jeshi la Polisi mjini Tehran ilitangaza kuwa Mahsa Amini, alipelekwa kituo kimoja cha polisi  hapo Tehran kwa ajili ya kupatiwa maelezo na mafunzo kuhusu umuhimu wa kuzingatia Hijabu lakini akapata tatizo la moyo na kukimbizwa hospitalini mara moja kwa ushirikiano wa polisi na kitengo cha huduma za dharura, lakini kwa bahati mbaya alifariki dunia. Maadui wametumia kifo hicho kuchochea ghasia na machafuko nchini Iran.

Khatibu wa Sala ya Ijumaa Tehran amesema, viongozi wote wa ngazi za juu humu nchini wamechukua hatua za kufuatilia kifo hicho na hilo linaonesha ni kiasi gani viongozi hao wana huruma na wananchi wao. Ameongeza kuwa, kwa muda mrefu adui wa taifa la Iran alikuwa anatafuta fursa ya kuchochea machafuko lakini alikuwa ameshindwa. Amesisitiza kuwa, kisingizio kilichotumiwa na wafanya fujo hao ni cha ajabu sana hasa kutokana na kuwa viongozi wakuu humu nchini wako mstari wa mbele kushughulikia kifo cha Mahsa Amini na hakuna sababu yoyote ya kufanya vurugu.

Baada ya khutba hiyoi, wananchi wanamapinduzi wa Tehran na Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, wamefanya maandamano hayo makubwa kote nchini ili kuwaonesha maadui kuwa wahalifu hao hawawakilishi hata asilimia ndogo tu ya wananchi wa taifa hili la Kiislamu.

Wakati huo huo, Wananchi wa Tehran na wa maeneo mengine yote ya Iran leo baada ya Sala za Ijumaa, wameshiriki kwa wingi katika maandamano makubwa ya kulaani magenge ya wanaofanya fujo, kuchoma mali za uma, kuvunjia heshima matukufu ya kidini na kijamii ya wananchi wa Iran.

Wakati wananchi wengi wa Iran wameguswa na kusikitishwa na kifo cha Mahsa Amini na hivi sasa wanasubiri kutangazwa rasmi matokeo ya uchunguzi wa sababu ya kifo chake, imefanyika mikusanyiko ya malalamiko na upinzani katika baadhi ya miji ukiwemo wa Tehran ambayo imesababisha uharibifu wa mali za umma.

Ijapokuwa idadi ya wanaofanya fujo ni ndogo na licha ya kwamba wafanya fujo hao ni wale wale wenye historia ya kushiriki katika maandamano ya fujo kila yanapotokea, lakini vyombo vya habari vya maadui wa taifa la Iran vinakuza kupindukia matukio hayo na kudai kuwa wahalifu hao wanawakilisha wananchi wa Iran.

4087415

captcha