Vyombo vya habari vimeripoti kuwa, Fat-hi Nurin, mwanamichezo wa Judo kutoka Algeria alitangaza kujiondoa kwenye michuano ya Olimpiki baada ya kura ya duru ya pili ya utangulizi wa mashindano hayo katika uzito wa chini ya kilo 73 kumwangukia apambane na mshindani kutoka Israel.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, Nurin, ambaye ni bingwa wa uzito huo nchini Algeria amechukua uamuzi huo wa kishujaa wa kukubali kukosa kushiriki mashindano makubwa zaidi ya michezo duniani ili kulalamikia hatua ya baadhi ya nchi za Kiarabu ya kuanzisha uhusiano wa kawaida na utawala wa Kizayuni na vilevile kuonyesha mshikamano na wananchi madhulumu wa Palestina.
Algeria, kinyume na jirani yake Morocco, ni nchi inayopinga kuanzisha uhusiano wa aina yoyote na utawala haramu wa Israel na kuendelea kushikilia kila mara msimamo wake thabiti wa kuliunga mkono taifa la Palestina.
Katika miezi ya karibuni, nchi za Imarati, Bahrain, Sudan na Morocco zimechukua hatua ya kutangaza hadharani uamuzi wao wa kuanzisha uhusiano wa kawaida na utawala wa Kizayuni, uamuzi ambao umekabiliwa na malalamiko makubwa na upinzani mkali wa makundi ya muqawama ya Palestina.