Akizungumza na IQNA, Badriya al-Abduli alisema utaratibu na nidhamu katika kuandaa mashindano hayo unaweza kuwa mfano kwa nchi za Kiislamu.
Pia alisifu maendeleo yanayoonekana kila mwaka katika mashindano ya kimataifa ya Qur'ani ya Iran, na kusema kila kitu katika mashindano ya mwaka huu kimefanyika kwa nidhamu na mpangilio bora.
Kwa upande wa jopo la waamuzi au majaji, alisema kulikuwa ushirikiano mzuri kati ya wataalam wote walioohudumu katika jopo hilo na alama zilizotolewa kwa washindani zina usawa.
Pia alipongeza kiwango kizuri cha washiriki katika sehemu ya wanawake.
Akizungumzia kauli mbiu ya mashindano hayo ambayo ni “Kitabu Kimoja, Umma Mmoja”, alisema kauli mbiu hiyo ni hitajio la dharura kwa ulimwengu wa Kiislamu hivi leo wakati ambapo kuna mashambulizi ya aina tofauti dhidi ya Uislamu na maadui wanataka kuchochea Fitna miongoni mwa Waislamu.
Katika hali kama hizo, Waislamu wanapaswa kuwa na umoja na kutoegemea Mashariki na Magharibi, kama muasisi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran hayati Imam Khomeini (RA) alivyosema, mtaalamu huyo wa Qur'ani alisisitiza.
Kwingineko katika matamshi yake, al-Abduli alionyesha matumaini kwamba juhudi zitafanywa kuwavutia wanawake wengi zaidi wa Kiislamu kwenye shughuli za Qur'ani ili waweze kukabiliana na mashambulizi ya kitamaduni ya Magharibi na majaribio ya kuwapoteza vijana.
Duru hii ya mashindano ya kimataifa ya Qur'ani ilifanyika katika hatua mbili, ambapo duru ya kwanza ilifanyika kwa njia ya intaneti miezi kadhaa iliyopita na kushirikisha wagombea 150 kutoka nchi 80.
Kutoka miongoni mwao, maqari wa Qur'ani na waliohifadhi Qur'ani kutoka nchi 33 walifika kwenye fainali iliyofanyika mjini Tehran Februari 18-22. Mashindano hayo yalifunguliwa sambamba na mnasaba wa kukumbuka Kubaathiwa au kupewa utume, Mtume Muhammad SAW.
Kauli mbiu ya mashindano ya mwaka huu, kama lile lililotangulia, ni "Kitabu Kimoja, Umma Mmoja", jambo ambalo linaashiria Jamhuri ya Kiislamu ya Iran inalipa umuhimu mkubwa umoja na udugu kati ya mataifa ya Kiislamu.
4123652